Ngara yaongoza kwa Vifo vya Uzazi mkoani Kagera. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Friday, May 18, 2018

Ngara yaongoza kwa Vifo vya Uzazi mkoani Kagera.

 Wananchi wa Kihinga,wilayani Ngara mkoani Kagera.

 Jamii imetakiwa kuweka akiba ya fedha kwa Kaya zao zenye wanawake wajawazito wanaohitaji kujifungua ili kuepukana na vifo ambavyo vinachangia kupunguza nguvu kazi ya familia na taifa kwa ujumla.

 Wito huo umetolewa May 17,2018 na mratibu wa taifa wa muungano wa utepe mweupe wa uzazi salama, Rose Mlayi kwenye mkutano wa kijiji cha kihinga wilaya ya Ngara mkoani Kagera na kwamba fedha hizo zitasaidia kumhudumia mjamzito ikiwemo kwenda kujifungua kituo cha afya. 

Mlayi alisema wanawake wajawazito 100,000 wanaokuwa katika harakati za kujifungua nchini Tanzania kati yao 11,000 wanapoteza maisha kwa mwaka kwa sababu ya maandalizi duni wakati wa ujauzito ambapo wanawake 30 hufariki kila siku wakati wa kujifungua.

 Alisema viongozi wa vijiji na wataalamu wa Afya nchini hawana budi kuhamasisha jamii kutokomeza vifo vya akina mama wanaojifungua pamoja na kuhimiza kuwahi kliniki wakiwa na wanaume wao kupata ushauri wa kutunza mtoto aliyeko tumboni.

Alisema Mlayi ameeleza wilaya ya Ngara inaongoza kwa vifo vya uzazi katika mkoa wa Kagera ambapo kwa mwaka jana 2017 walifariki Wanawake 7 ambapo kati ya hao kijiji cha Kihinga kimepoteza wawili wakati wakijifungua kwa kuchelewa kuwahi vituo vya Afya ngazi ya kijiji. 

Katika mkutano huo wakazi wa kijij cha Kihinga ,Kata ya Kibogora walisema changamoto kubwa inayochangia vifo kutokea ni umbali wa kutoka kwenye vitongoji wanakoishi hadi zahanati na vituo vya Afya viko umbali mrefu.
Diwani wa Kata ya Kibogora Adroniz Bulindoli.

Aidha Diwani wa Kata ya Kibogora Adroniz Bulindoli alisema kijiji cha Kihinga chenye wakazi 7988 wanaishi katika kaya 1884 ndani ya vitongoji vitano wanatumia Zahanati moja iliyo na uwezo wa kuhudumia watu 4,535 na kwamba hulazimika  kulipia Shilingi  10,000 kusafirisha mjamzito kutoka kijijini humo hadi kituo cha Afya Bukiriro kilicho umbali kilomita 12 au Shilingi  50,000 kwenda Hospitali ya misheni ya Rulenge.

Wamama wa Kihinga wilayani Ngara mkoani Kagera wakitoa burudani wakati wa mkutano huo.

Hata hivyo Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Ngara, Gidion Mwesiga alisema mkakati wa kupunguza vifo kwa wilaya hiyo umeanza baada ya Serikali kutoa Shilingi milioni 800 kuboresha kituo cha Afya Mabawe na Murusagamba sambamba na vituo vingine vitakavyo boreshwa ni Bukiriro, Lukole, kisha kujenga kituo kipya Kata ya Rusumo na kwamba zaidi ya zahanati za vijiji 16 zimefikia hatua mbalimbali za ujenzi.

 Mgeni rasmi katika mkutano huo, Mkuu wa wilaya ya Ngara Michael Mntenjele alisema serikali inaendelea kutafuta fedha kijenga miundombinu katika sekta za afya, hivyo wajawazito wajitahidi kuwahi vituo vya kutolea huduma kuepukana na vifo visivyo vya lazima.


Picha Na-RADIO KWIZERA.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad