Mamalaka ya
Mapato Tanzania (TRA) imesitisha utoaji wa huduma za usafiri kwa kampuni ya
mabasi ya Kilimanjaro Express Limited baada ya kushindwa kulipa kodi ya Sh500
milioni.
Akizungumza
na gazeti la Mwananchi, Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi wa TRA,
Richard Kayombo amesema wamefikia uamuzi huo baada ya majadiliano ya muda mrefu
na kampuni hiyo kutokuzaa matunda.
Kayombo amesema
biashara ya mmiliki huyo kwa kipindi cha hivi karibuni haikuwa nzuri kwani
mabasi yake 26 yalipungua hadi kufikia 12 lakini si kigezo cha kutokulipwa kwa
kodi ya Serikali.
“Ni kweli
Kilimanjaro Express inadaiwa Sh500 milioni jambo ambalo lilitufanya sisi
kusimamisha shughuli tangu Jumatatu (ya Novemba 13) hadi hapo atakapolipa kodi
anayodaiwa,” amesema Kayombo
Kwa upande
wake, mmiliki wa kampuni hiyo, Roland Sawaya amesema wamezuia mabasi yake
ambayo yalikuwa yameegeshwa katika ghala mjini Moshi mkoani Kilimanjaro huku
akieleza kuwa ni kweli anadaiwa lakini amekuwa akilipa deni hilo kwa awamu.
Amesema hivi
karubuni alilipa Sh50 milioni na mwezi huu walitaka kulipa Sh35 milioni lakini
TRA walikataa na kuwataka kulipa kiasi chote kilichobaki cha Sh500 milioni huku
akieleza kwamba mazungumzo yanayoendelea ana imani yatafikia mwafaka na kurejea
kutoa huduma
Kilimanjaro
ambayo imekuwa ikifanya safari zake kati ya Dar es Salaam, Moshi na Arusha kwa
zaidi ya miaka 20 ni kampuni tanzu ya Kilimanjaro Cargo Truck.
|
No comments:
Post a Comment