Baadhi ya
wabunge wa mabunge ya Uingereza wakiwa katika kikao na Waziri wa Fedha na
Mipango, Mhe. Dkt, Philip Isdor Mpango (Mb) (hayupo pichani), katika ukumbi wa
Wizara ya Fedha na Mipango Jijini Dar es Salaam.
|
Waziri wa
Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (kushoto), akisisitiza
jambo alipokutana na kufanya mazungungumzo na wabunge kutoka nchini Uingereza
waliomtembelea Jijini Dar es Salaam.
Kulia kwake ni Kaimu Kamishna wa Fedha za
Nje, Wizara ya Fedha na Mipango, Bi. Mamelta Mutagwaba.
|
Waziri wa
Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (wa pili kushoto) na
Kiongozi wa Ujumbe wa Wabunge kutoka Uingereza, Mhe. David Linden (katikati) na
Wabunge wengine kutoka Uingereza, Maafisa Waandamizi kutoka Tanzania, wakiwa
katika picha ya pamoja baada ya kumalizika kwa Mkutano katika Ukumbi wa Wizara
ya Fedha na Mipango Jijini Dar es Salaam.
(Picha na Kitengo cha
Mawasiliano Serikalini-Wizara ya Fedha na Mipango)
Benny Mwaipaja, WFM, Dar es Salaam.
Tanzania imetoa
rai kwa Serikali ya Uingereza kubadili mfumo wa uhusiano wake kwa kujikita
zaidi katika masuala ya biashara na uwekezaji badala ya kutoa misaada ya
kawaida ili nchi iweze kukuza uchumi wake kwa haraka zaidi.
Wito huo
umetolewa Jijini Dar es Salaam na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Isdor
Mpango, alipokutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa wabunge kutoka mabunge
ya uingereza (Baraza la Mamwinyi na Bunge la Wawakilishi).
Dokta Mpango
amesema kuwa kiwango cha mtaji ambacho Serikali ya Uingereza imewekeza nchini
hadi sasa ni Paundi bilioni 2.5 lakini kwa upande wa biashara kati ya nchi hizo
mbili, hali si nzuri.
"Mwaka
2015 Tanzania iliuza nje bidhaa zenye thamani ya Dola za Marekani milioni 22.5
na kununua bidhaa kutoka Uingereza zenye thamani ya Dola milioni 150, kiwango
ambacho ni kidogo sana na tunahitaji kufanya biashara zaidi" Alisisitiza
Dkt. Mpango.
Alielezea
hatua mbalimbali ambazo Serikali inazichukua kuimarisha uchumi wa viwanda na
kuelezea changamoto kubwa ikiwa na namna ya kuendeleza kilimo kwa ajili ya
kupata malighafi za viwanda na kuwainua wananchi kiuchumi kwa kuwa kilimo
ndicho kinaajiri idadi kubwa ya Watanzania.
Dkt. Mpango
alitoa wito kwa Serikali ya Uingereza kuwekeza zaidi katika viwanda
vitakavyoongeza thamani ya bidhaa mbalimbali ikiwemo kujenga viwanda vya
kutengeneza matrekta na zana nyingine za kilimo, kusindika bidhaa za mazao ya
wakulima pamoja na kuwekeza katika sekta za kuongeza thamani ya madini na
nishati ya umeme.
Dokta Mpango
aliwaeleza Wabunge hao kwamba hivi sasa Serikali imepiga hatua kubwa kiuchumi
na kuishukuru Uingereza kwa mchango mkubwa inaoutoa kusaidia Elimu, Lishe,
Maboresho ya Usimamizi wa Fedha za Umma na afya kwa upande wa lishe, uwekezaji
ambao kwa pamoja umefikia zaidi ya paundi milioni 180.
Kwa upande
wake, kiongozi wa Wabunge watano waliomtembelea Waziri wa Fedha na Mipango,
Mheshimiwa David Linden, amesema wamefurahishwa na namna Tanzania inavyopiga
hatua kubwa kimaendeleo na kudhibiti vitendo vya rushwa.
Amesema kuwa
wameridhishwa na kiwango cha miradi wanayoifadhili katika sekta ya elimu na
afya hususan masuala ya lishe kwa watoto na kwamba nchi yao itaendelea
kuisaidia Tanzania ili iweze kufikia malengo yake kiuchumi na kijamii
Wabunge hao
wapo nchini tangu Jumapili iliyopita na wanatembelea miradi mbalimbali
inayofadhiliwa na Serikali ya Uingereza.
|
No comments:
Post a Comment