Maafisa
waandamizi kutoka Tanzania wakifuatilia kwa makini Mkutano wa Mashauriano ya
Kimaendeleo kati ya Tanzania na Ujerumani yaliyofanyika katika ukumbi wa Wizara
ya Fedha na Mipango Jijini Dar es Salaam.
|
Wajumbe
kutoka Ujerumani waliohudhuria Mkutano wa Mashauriano ya Maendeleo kati ya
Tanzania na nchi hiyo wakisililiza kwa makini maelezo ya Naibu Katibu Mkuu wa
Wizara ya Fedha na Mipango Bi. Amina Khamis Shaaban (hayupo pichani) akieleza
mafanikio ya msaada wa nchi hiyo katika Nyanja za Afya, Maji, Nishati na
Utawala wa Fedha, katika ukumbi wa Wizara ya Fedha na Mipango Jijini Dar es
Salaam.
Ujerumani
imeipatia Tanzania kiasi cha Euro milioni 198.5 sawa na Sh. Bilioni 520.86 zilizotumika kufadhili miradi mbalimbali
ikiwemo ya Maliasili na Mazingira, Afya, Maji, Nishati, Udhibiti wa Fedha za
Umma (Good Financial Governance) na Kusaidia Huduma za Wakimbizi katika mkoa wa
Kigoma, katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.
Hayo
yamesemwa Jijini Dar es Salaam na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na
Mipango, Bi. Amina Khamis Shaaban wakati wa tukio la Tanzania na Ujerumani
kusaini kumbukumbu za Mkutano wa Mashauriano ya Kimaendeleo (Bilateral
Development Consultations) ambapo Ujerumani imeonesha nia ya kuendelea
kuisaidia Tanzania katika Sekta hizo kuanzia mwaka 2018 hadi 2021.
Kumbukumbu
za Mashauriano hayo zimesainiwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na
Mipango Bi. Amina Khamis Shaaban kwa
niaba ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Naibu Mkuu wa Idara ya
Kanda ya Afrika Mashariki katika Wizara ya Ushirikiano wa Kiuchumi na Maendeleo
ya Ujerumani Bw. Georg Rademacher kwa
niaba ya Serikali ya Ujerumani.
Mkutano huo
ni maandalizi ya mkutano wa Majadiliano ya Kimaendeleo (Bilateral Negotiations)
kati ya nchi hizi mbili unaotarajiwa kufanyika mwaka 2018 ambapo Serikali ya
Ujerumani itatangaza kiasi cha fedha watakazotoa kama msaada kwa ajili ya
kufadhili Sekta zilizoainishwa katika kumbukumbu zilizosainiwa.
“
Tunaishukuru Ujerumani kwa kuwa miongoni mwa washirika wa muda mrefu wanaotoa
misaada mikubwa ya kimaendeleo kwa Tanzania na sisi tunaahidi kuendeleza ushirikiano
huo kwa faida ya pande zote mbili” alisema Bi. Amina Khamis Shaaban.
Kwa upande
wake Bw. Georg Rademacher kwa niaba ya Serikali ya Ujerumani amesema kwamba
Tanzania imekuwa na sifa njema nchini Ujerumani hasa kwa sababu ya amani
iliyopo, jinsi ambavyo imehifadhi maliasili zake na kuifanya kuwa nchi yenye
vivutio vya kipekee vya utalii.
Bwana
Rademacher aliongeza kwamba kwa sasa nchi ya Tanzania imepiga hatua kubwa sana
katika kupambana na ubadhirifu wa mali za Umma na kwamba Ujerumani itaendelea
kuisaidia Tanzania ili kuweza kuleta maendeleo kwa watu wake na kuondoa
umaskini.
Imetolewa
na;
Benny
Mwaipaja
Mkuu wa
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
Wizara ya
Fedha na Mipango
|
No comments:
Post a Comment