Tume ya
Taifa ya Uchaguzi (NEC) imefafanua juu ya uteuzi wa wabunge wapya wa Viti
Maalumu wa Chama cha Wananchi (CUF).
Imesema kuwa
imesikitishwa na kushangazwa na taarifa za Baraza Kuu la Taifa la chama hicho
kwamba tume hiyo imekiuka kanuni zake katika uteuzi wa wabunge wanane wa chama
hicho ili kujaza nafasi za wazi zilizotokea hivi karibuni.
Aidha,
imesema chama husika kilipewa fursa ya kupendekeza na kilifanya hivyo, kabla ya
NEC kuanika majina ya wabunge wapya wa CUF katika Bunge la Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania.
Hayo yamo
katika taarifa ya Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Bw.Kailima Ramadhani aliyoitoa
jana jioni, akizungumzia tuhuma dhidi ya tume hiyo, inayodaiwa kukiuka kanuni
katika uteuzi wa wabunge wanane wa viti maalumu wa CUF.
Sehemu ya
Taarifa ya CUF katika mitandao ya kijamii inayoituhumu NEC inasema; “Kanuni
walizojiwekea wenyewe Tume katika uteuzi wa watu wa kujaza nafasi hizo zinasema
uteuzi huo unafuata mpangilio wa majina, kama ulivyokuwa umewasilishwa na chama
husika wakati wa uteuzi wa wagombea wa ubunge wa viti maalumu wakati wa
uchaguzi mkuu uliopita.
“CUF
ilipeleka orodha yake ambayo haihusishi majina yaliyotangazwa, hivyo ndiyo
kusema hata kama hicho kinachoitwa kufukuzwa uanachama wabunge hao kingekuwa
halali (jambo ambalo si halali kama ilivyokwishaelezwa hapo juu), basi kwa
Kanuni za Tume yenyewe, watu wa kujaza nafasi hizo wasingekuwa hao
waliotangazwa.”
Bw.Kailima,
katika taarifa yake, alisema taarifa zinazotolewa katika mitandao zikihusisha
NEC kukihujumu chama hicho ni za kushangaza na kwamba Baraza Kuu la Uongozi la
CUF, linataka kuupotosha umma kuhusu utekelezaji wa kazi za Tume.
“Chama
husika ndicho kinaweza kujua ni nani siyo mwanachama wa chama hicho kwa kipindi
cha kujaza nafasi wazi inapotokea,” alieleza Kailima na kuongeza kuwa, kwa
mujibu wa majina manane yaliyopendekezwa na CUF kujaza nafasi wazi za wabunge
wa viti maalumu ni miongoni mwa majina 55 yaliyowasilishwa na chama hicho kwa
barua yenye kumbukumbu Namba CUF/AK/DSM/ KM/003/1A/2015/14 ya Septemba 28, 2015
iliyosainiwa na Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Shariff Hamad.
|
No comments:
Post a Comment