Waziri wa
Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe amesema kuanzia mwezi Julai mwaka
huu hakuna mkaa wowote utakaosafirishwa kutoka wilaya moja kwenda nyingine ili
kunusuru misitu inayoteketea nchini.
Waziri huyo
ameyasema hayo wakati akifungua mkutano wa 24 wa baraza la wafanyakazi wa
Wizara ya Maliasili na Utalii uliofanyika katika ukumbi wa LAPF mjini Dodoma
uliohudhuriwa na wajumbe mbalimbali kutoka kwenye vitengo na Taasisi mbalimbali
zilizopo chini ya Wizara hiyo.
“Kuanzia
mwezi Julai hakuna ruhusa ya kutoa vibali vya kuhamisha mkaa kutoka wilaya moja
kwenda wilaya nyingine, mkaa utachomwa, utauzwa ndani ya wilaya kwa ajili ya
matumizi ya watanzania wanaohitaji nishati ya mkaa, lakini biashara ya mkaa ya
kutoa Dodoma kwenda Dar es Salaam mpaka Zanzibar marufuku,” alisema Maghembe.
“Wamekata
misitu yetu yote, mito yetu imekauka, tunashindwa kupata maji ya umwagiliaji
kwasababu watu wengi huko nje wanataka mkaa wetu, Tanzania jamani sio shamba la
bibi, wale wote watakaotoa mkaa kutoka eneo moja hadi jingine kinyume na sheria
hii watashuulikiwa kwa utaratibu wa uhujumu uchumi”, amesema Maghembe.
Aidha
alisema kwa upande wa miji mikubwa kama Dar es Salaam, Dodoma, Morogoro na
Tanga vitaanzishwa viwanda maalumu vya kuzalisha mkaa ambao utauzwa kwa vibali
maalumu katika mikoa mbalimbali hapa nchini.
Amesema mkaa huo hautakuwa na
athari nyingi za kimazingira kwa sababu utazingatia taratibu za uzalishaji
endelevu.
|
No comments:
Post a Comment