Halmashauri zabebeshwa zigo la Magari ya Wagonjwa. - Mwana Wa Makonda

Muhtasari

X-BET


Post Top Ad

Friday, April 21, 2017

Halmashauri zabebeshwa zigo la Magari ya Wagonjwa.

Serikali imesema katika miaka miwili ya 2016/17 na 2017/18, haijatenga fedha kwa ajili ya ununuzi wa magari ya wagonjwa.
 
Kauli hiyo ilitolewa na Naibu Waziri Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Hamisi Kigwangalla alipojibu swali la Mbunge wa Mafinga Mjini (CCM), Cosato Chumi. 
Mbunge huyo alitaka kujua ni lini Serikali itapeleka mapendekezo ya kubadilisha sheria ya fedha ili magari hayo yaingie kwenye jedwali la saba, hivyo kupata msamaha wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (Vat).
 
Chumi alisema katika mwaka wa fedha 2016/17, Serikali haina mpango wa kununua magari hayo na jukumu hilo limeachiwa halmashauri za wilaya ambazo hazimudu.
 
Dk Kigwangalla alisema katika mwaka wa fedha 2016/17, wizara haikutengewa fedha za kununua magari na hata makadirio ya fedha ya mwaka 2017/18 fedha hizo hazipo.
 
Alisema wizara pindi inapopata misaada kutoka kwa wadau mbalimbali wa maendeleo, imekuwa ikigawa magari hayo katika halmashauri nchini kwa kuzingatia mahitaji.
 
Hata hivyo, Dk Kigwangalla alisema Sheria ya Kodi ya mwaka 2014, jedwali la saba imeeleza ununuzi wa vifaatiba utapatiwa msamaha baada ya kuridhiwa na waziri mwenye dhamana ya afya na kwamba hata magari hayo huombewa msamaha.
 
Kuhusu suala la Vat katika magari hayo, Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Ashatu Kijaji alisema Serikali tayari imeona changamoto hiyo na imeanza kuifanyia kazi.
 
Dk Kijaji alisema katika sheria mpya ijayo ya fedha jambo hilo litapatiwa ufumbuzi, hivyo aliwataka wabunge kuwa na subira.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad