Aliyekuwa
Mkurugenzi wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) Nchini
Tanzania, Dk Mwele Malecela ameteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Vituo vya Kudhibiti
na Kuzuia Magonjwa Afrika vya Shirika la Afya Duniani (WHO), Kanda ya Afrika.
Pia, Dk
Mwele aliteuliwa kuwa Mwenyekiti wa
Mpango wa Maalumu wa WHO wa kutokomeza magonjwa yasiyopewa kipaumbele (ESPEN)
na sasa atahamia kituo chake cha kazi Congo-Brazaville.
Mradi wa ESPEN
ulianza kutekelezwa mwaka 2016 hadi 2020, una lengo la kumaliza magonjwa
yasiyopewa kipaumbele kwa kutoa vifaa tiba, elimu na dawa.
Magonjwa
yasiyopewa kipaumbele ni pamoja na matende, mabusha, kichocho, minyoo ya tumbo
na usubi.
Miongoni mwa
waliomtumia pongezi ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Afya ya Sikika, Irenei Kiria
ambaye aliandika katika ukurasa wake wa Twitter: “Hongera Mwele kwa kupata
nafasi hiyo ina maana ulipangwa kulisaidia Taifa letu ukiwa nje.”
Mwingine ni Mhadhiri wa Saikolojia wa Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Kitila Mkumbo aliyeandika katika ukurasa wake
wa twitter akisema: “Nina furaha kwa uteuzi wa Dk Mwele kuwa Mkurugenzi wa
WHO.Nahisi kusamehewa kwa kuikosoa Serikali baada ya kumuondoa NIMR.”
Mbunge wa
Kigamboni, Dk Faustine Ndugulile yeye aliandika katika ukurasa wake akimpongeza
Dk Mwele na kusema, “Nimezidiwa na furaha baada ya kupata taarifa kuwa umepata
kazi kubwa katika ogani ya kimataifa. Mlango mmoja ukifungwa mwingine
hufunguliwa. Katumikie vyema.”
Dk Mwele
aliondolewa kuwa Mkurugenzi wa NIMR na Rais wa Tanzania, Dkt.John Magufuli Desemba 17 mwaka
jana,2016.
Kuondolewa
kwake katika nafasi hiyo kulifanyika siku moja baada ya kutoa ripoti ya utafiti
wa magonjwa, ndani yake ikiwamo taarifa ya virusi vya ugonjwa wa Zika katika
maeneo ya Morogoro, Geita na Magharibi mwa Tanzania.
Taarifa ya
Dk Mwele, ilieleza kuwa kati ya watu 533 waliopimwa, asilimia 15.6 walibainika
kuwa na virusi hivyo.
Siku moja
baada ya kutoa takwimu hizo, Waziri wa Afya, Mhe.Ummy Mwalimu akiwa na Dk Mwele
aliitisha mkutano na waandishi wa habari kukanusha taarifa hizo kwamba ugonjwa
huo bado haujaingia nchini.
|
No comments:
Post a Comment