Aliyekuwa mwanachama
mkongwe wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake
Tanzania (UWT), Sophia Simba ambaye alifukuzwa uanachama kwa usaliti,
amezungumzia hatua aliyoichukua baada ya uamuzi huo dhidi yake.
Wikendi
iliyopita, CCM ilitangaza kumvua uanachama Mwanasiasa huyo baada ya kumtia
hatiani, ambapo taarifa zinadai kuwa yeye alibainika kwenda nyumbani kwa
aliyekuwa mgombea wa urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa hata baada ya
uchaguzi mkuu akiwa amevalia hijabu kujificha. Hali iliyotafsiriwa kuwa alikuwa
akimpelekea siri za chama.
Baada ya
uamuzi huo wa CCM kutangazwa, Lowassa alimkaribisha Sophia Simba na wenzake 12
waliofukuzwa, kujiunga na Chadema huku akiwaita mashujaa waliokuwa wanatetea
demokrasia ndani ya chama hicho tawala.
Hata hivyo,
Sophia Simba amesema kuwa hana mpango na hatahamia katika chama chochote kwani
maisha yake yote yametokana na kuitumikia CCM.
Mwanasiasa
huyo ambaye alijiunga na CCM tangu ilipozaliwa mwaka 1977 na kushika nyadhifa
mbalimbali baadae, amesema kuwa atabaki kuwa mkereketwa wa chama hicho.
“Napenda
kuwaeleza Watanzania wote, wafahamu kuwa sina mpango wowote wa kujiunga na
upinzani. Na unajua CCM ina makundi mawili, la kwanza ni wanachama wenye kadi
na la pili wakereketwa ambao ni wengi. Na mimi nitaingia katika kundi hilo na
sio kuhama,” Sophia Simba anakaririwa na Mtanzania.
Aidha,
alikanusha taarifa zilizokuwa zimeripotiwa kwenye baadhi ya mitandao kuwa
amekutana na mwanasiasa mmoja wa upinzani. Alisisitiza kuwa hakufanya hivyo na
hana mpango huo.
Akizungumzia
tuhuma za kukisaliti chama hicho zilizopelekea kung’olewa kwake, alikana kuwa
msaliti wa chama hicho ingawa alisisitiza kuwa hataki kulizungumzia kwa undani
bali anamuachia Mungu anayeiona nafsi yake.
“Sitaki
kuzungumzia kwa udani suala la usaliti ila kwa ufupi, Mungu anaishuhudia nafsi
yangu. Jamani, hivi kweli nikisaliti chama changu ambacho kimenilea katika
maisha yangu yote!”
Katika hatua
nyingine, alisema kuwa hana mpango wa kwenda mahakamani kutafuta haki ya
kurejea ndani ya chama hicho kwani kufanya hivyo ni kukosa fadhila kwa jinsi
ambavyo chama hicho kimempa maisha.
Mwanasiasa
huyo mkongwe alisema kuwa amepokea adhabu aliyopewa kwa mikono miwili na kwamba
hana kinyongo.
|
No comments:
Post a Comment