Rais na
Amiri Jeshi Mkuu Dkt John Pombe Magufuli akijiandaa kufyatua risasi ya bastola
kuashiria matumizi rasmi ya Uwanja wa kisasa wa ndegevita wa Ngerengere mkoani
Morogoro Jana Machi 6, 2017.
|
Rais na
Amiri Jeshi Mkuu Dkt John Pombe Magufuli na Balozi wa China nchini Dkt. Lu
Youqing katika picha ya pamoja na viiongozi mbalimbali baada ya uzinduzi rasmi ya Uwanja wa kisasa wa ndegevita
wa Ngerengere mkoani Morogoro.
|
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, hapo jana tarehe 06 Machi, 2017 amezindua uwanja wa kisasa wa ndegevita wa Ngerengere uliopo Mkoani Morogoro, uliofanyiwa ukarabati mkubwa baada ya miundombinu ya uwanja uliojengwa tangu mwaka 1970 kuharibika.
Sherehe ya uzinduzi wa uwanja huo imefanyika uwanjani hapo na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Balozi wa China hapa nchini Mhe. Dkt. Lu Youqing, Viongozi wa vyombo vya ulinzi na usalama na Wakuu wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania wastaafu.
|
Mkuu wa
Majeshi ya Ulinzi Jenerali Venance Salvatory Mabeyo amesema ukarabati wa uwanja
huo ulioanza tarehe 15 Julai, 2013 umegharimu Shilingi Bilioni 137 na Milioni
631 ikiwa ni ufadhili wa Serikali ya China na umehusisha kujenga upya njia ya
kuruka na kutua ndege yenye urefu wa mita 3,000 upana wa mita 45 na unene wa
sentimeta 45 pamoja na maegesho ya ndege za kivita na ndege za abiria.
Jenerali
Mabeyo ameongeza kuwa uwanja huo ni miongoni mwa viwanja bora zaidi duniani kwa
sasa na una uwezo wa kutumiwa na ndege za aina zote zilizo chini ya Boeing 777
huku akibainisha kuwa pamoja na ndege za kivita pia unaweza kutumiwa na ndege
za kawaida za abiria kwa dharula.
Nae Balozi
wa China hapa nchini Mhe. Dkt. Lu Youqing amesema kujengwa kwa uwanja huo
kumeimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na China na
amempongeza Mhe. Rais Magufuli kwa kuendeleza uhusiano huo.
Pamoja na
kuzindua uwanja huo, Mhe. Rais Magufuli ameshuhudia maonesho ya ndege za kivita
zilizorushwa kwa mbinu mbalimbali za kivita, kutoa heshima na kutua katika
uwanja huo.
Katika
hotuba yake, Mhe. Rais Magufuli amelipongeza Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa
Tanzania (JWTZ) kwa kazi kubwa linayofanya na pia amemshukuru Rais wa Jamhuri
ya Watu wa China Mhe. Xi Jinping na Serikali yake kwa msaada mkubwa iliyoutoa
kujenga uwanja huo.
“Mhe. Balozi
Lu Youqing naomba unipelekee shukrani zangu za dhati Mhe. Rais wa China kwa
kutoa msaada huu mkubwa wa kujenga uwanja wa ndegevita wa Ngerengere, najua
China imetusaidia kujenga Reli ya TAZARA, Kiwanda cha Urafiki na Uwanja wa
Mpira, hii yote inathibitisha uhusiano wetu mzuri, urafiki na undugu” amesema
Mhe. Rais Magufuli.
Aidha, Mhe.
Dkt. Magufuli ameahidi kujenga barabara ya lami ya kuunganisha Kamandi ya Jeshi
la anga ya Ngerengere na barabara kuu ya Dar es Salaam – Morogoro.
|
No comments:
Post a Comment