Aliyekuwa
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo wa Tanzania, Nape Nnauye amesema ataendelea
kuwa mtiifu kwa Rais John Magufuli, Serikali na Chama cha Mapinduzi tofauti na
maneno yanayosemwa mitandaoni.
Tangu
alipoachwa kwenye mabadiliko madogo ya Baraza la Mawaziri, Machi 23,2017 kumekuwa
na taarifa nyingi feki kwenye mitandao ya kijamii kuhusu kuenguliwa kwake
zikidaiwa kutolewa na mbunge huyo wa Mtama ambazo hata hivyo, amekuwa
akizikanusha.
Akizungumza
jana wakati akikabidhi ofisi kwa waziri mpya wa wizara hiyo, Dk Harrison
Mwakyembe katika ofisi za wizara hiyo mjini hapa, bila kutaja maneno hayo ya
mitandaoni, Nape alisema ataendelea kumuunga mkono Rais katika dhamira yake
njema ya kuleta mageuzi nchini.
“Heshima
aliyonipa Rais ni kubwa mno na nitaendelea kumuunga mkono katika dhamira yake
njema ya kuleta mageuzi nchini” alisema.
Alimshukuru
Rais kwa kumpa dhamana ya kusimamia wizara hiyo kwa miezi 15 baada ya
kuchaguliwa kuwa mbunge kwa mara ya kwanza. “Nitaendelea kutoa ushirikiano kwa
wizara hii kwa sababu mimi ni mdau mkubwa wa sekta hiyo,” alisema.
Waziri
Mwakyembe alisema ataendeleza mazuri yote yaliyofanywa na Nape katika
kuimarisha wizara hiyo na atahakikisha wizara hiyo inakuwa ya mfano nchini.
Alimsifu
Nape akisema katika kipindi kifupi alichokaa katika wizara hiyo amefanya
mabadiliko na watu wameanza kuifahamu.
Nape aliondolewa
katika nafasi hiyo siku moja baada ya kamati aliyounda kuchunguza tukio la
kuvamiwa kwa ofisi za Clouds kumkabidhi ripoti.
Mara baada
ya kupewa ripoti hiyo, Nape aliahidi kuikabidhi kwa mamlaka zake za juu
akizitaja kuwa ni Waziri Mkuu, Makamu wa Rais na Rais lakini asubuhi ya siku
iliyofuata aliondolewa katika nafasi hiyo.
Makabidhiano
hayo yalishuhudiwa na viongozi wengine wa Wizara hiyo, Naibu Waziri, Anastazia
Wambura, Katibu mkuu, Profesa Elisante Ole Gabriel na Naibu katibu mkuu, Nuru
Millao.
HAPA BOFYA
KUMSIKILIZA NAPE AKIONGEA.
|
No comments:
Post a Comment