Na Hamza
Temba - WMU
___________________________________________________________
Wananchi
wanaozunguka hifadhi za misitu na wanyamapori nchini wametakiwa kutii sheria za
uhifadhi na kujiepusha na vitendo viovu vya uharibifu wa mazingira
vinavyopelekea kupotea kwa uoto wa asili na kutishia nchi kuwa jangwa ambapo
pamoja na mambo mengine wametakiwa kuondoa mifugo yao katika maeneo
yaliyohifadhiwa kisheria.
Hayo
yamesemwa Oktoba 18,2016, Mkoani Geita na Naibu Waziri, Wizara ya Maliasili na
Utalii, Mhandisi Ramo Makani wakati akizungumza na viongozi na watendaji wa
Mkoa huo Wilayani Chato kuhusu maelekezo ya kuwaondoa wananchi waliovamia
maeneo hifadhi Mkoani humo na taifa kwa ujumla.
Alieleza
kuwa vitendo hivyo vya uharibifu wa mazingira ni pamoja na ukataji wa miti
hovyo, kilimo kisichoendelevu, uchungaji holela wa mifugo, uanzishaji makazi na
shughuli zingine za kibinadamu katika maeneo yaliyohifadhiwa kisheria ikiwemo
Hifadhi za Misitu, Mapori ya Akiba, Mapori Tengefu na Hifadhi za Taifa.
"kwa
sasa Tanzania inapoteza takriban hekta 372,000 za uoto wa asili kila mwaka na
endapo hali hiyo ikiachwa iendelee tishio la kutoweka kwa uoto huo ni kubwa
zaidi. Takwimu pia zinaonyesha kuwa Tanzania ina eneo la uoto wa asili lenye
ukubwa wa takriban Hekta milioni 48.1 na kwamba kasi hiyo ikiachwa iendelee
itaiacha Tanzania bila uoto wa asili baada ya miaka 129" alisema Makani.
Akizungumzia
taratibu za kuwaondoa wananchi katika maeneo yaliyohifadhiwa kisheria alisema
watumishi na viongozi wote wa Serikali wanaotekeleza zoezi hilo wanatakiwa
kufuata sheria na miongozo iliyowekwa ikiwa ni pamoja na kujiepusha na vitendo
viovu vinavyoweza kuichafua Serikali ikiwemo rushwa na unyanyasaji wa wananchi,
"watakaobainika kwenda kinyume na utaratibu huo watachukuliwa hatua za
kisheria" alisema.
Katika
utekelezaji na usimamizi wa sheria hizo za uhifadhi, aliwataka watumishi wa
Wizara ya Maliasili na Utalii kusimamia sheria hizo kila siku na kuendesha
utekelezaji wake kwa kushirikiana na kamati za ulinzi na usalama za Wilaya na
Mikoa ili kuimarisha utekelezaji wa sheria hizo na kuweka uwazi katika
utendaji.
Kwa upande
wa wananchi ambao wapo katika vijiji na vitongoji vilivyosajiliwa kisheria
aliwataka kutoanzisha au kuendeleza shughuli mpya za kibinadamu hususani
zinazosababisha uharibifu wa mazingira ikiwemo kuathiri mabadiliko ya tabia
nchi mpaka pale kikosi kazi cha kitaifa kitakapokamilisha kazi yake na
kuishauri Serikali namna bora ya kumaliza migogoro ya ardhi nchini.
Maagizo hayo
yamekuja ikiwa ni siku chache kabla ya kikosi kazi hicho ambacho kimeundwa na
Serikali kikiwa na wajumbe kutoka Wizara sita zinazohusika moja kwa moja na
changamoto mbalimbali za ardhi kwa madhumuni ya kufanya uchunguzi wa kina
ikiwemo kupitia sheria zote zinazohusika kabla ya kuishauri serikali namna bora
ya kumaliza migogoro ya ardhi ikiwemo kwenye maeneo ya hifadhi.
Makani
alizitaja wizara hizo kuwa ni Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Maliasili
na Utalii, TAMISEMI na Kilimo, Mifugo na Uvuvi ambazo ndizo zimeanza
utekelezaji wa zoezi hilo linalotarajiwa kukamilika mwezi Desemba mwaka huu.
Alisema Wizara nyingine mbili zitaungana baadae kukamilisha zoezi hilo ambazo
ni Maji na Umwagiliaji na Nishati na Madini.
Kwa upande
wake Mkuu wa Mkoa wa Geita, Meja Gen. Mstaafu Ezekiel Kyunga alisema Mkoa wake
unakabiliwa na uhaba wa ardhi uliosababishwa na ongezeko kubwa la watu
waliovutiwa na shughuli za kiuchumi Mkoani humo ikiwemo uchimbaji wa madini,
uvuvi, ufugaji pamoja na kilimo ambazo kwa namna moja ama nyingine imekuwa ni
changamoto kubwa katika uhifadhi Mkoani humo.
Alieleza changamoto nyingine kuwa
ni mitazamo tofauti ya baadhi ya wanasiasa kuhusu uhifadhi.
Naye Mkuu wa
Wilaya ya Chato, Bw.Shaaban Ntarambe alisema kumekuwepo na uharibifu mkubwa wa
misitu Wilayani humo ambapo Hifadhi ya Msitu wa Biharamulo - Kahama kwa upande
wa Wilaya yake umeharibiwa kwa asilimia 70 kutokana na shughuli za kilimo,
ufugaji, uchimbaji madini na makazi ya kudumu hali inayohatarisha kutoweka kwa
hifadhi hiyo.
Msitu wa
Biharamulo - Kahama una ukubwa wa hekta 134,684 na upo katika Wilaya tatu za
Chato, Bukombe na Biharamulo. Kwa upande wa Wilaya ya Chato ambapo
uharibifu huo umefanyika kwa asilimia 70
una ukubwa wa hekta 30,000.
|
No comments:
Post a Comment