Daudi Felix
Ntibenda jana,Agosti 18,2016, asubuhi alikuwa na majukumu ya kufungua mikutano miwili na
kufanya shughuli nyingine kwa nafasi yake ya mkuu wa Mkoa wa Arusha, lakini
hakuweza kuyatimiza kikamilifu majukumu hayo kwa kuwa Rais John Magufuli
alikuwa na mawazo tofauti na mipango yake.
Ingawa
haikufahamika sababu ya kuondolewa kwake, huenda mvutano baina yake na Umoja wa
Vijana wa CCM Mkoa ukawa umechangia.
Saa 2:12
asubuhi jana, Ofisi ya Waziri Mkuu ilikuwa imeshatoa taarifa kuwa uteuzi wa
Ntibenda umetenguliwa na nafasi yake imechukuliwa na Mrisho Gambo ambaye
aliteuliwa hivi karibuni kuwa mkuu wa Wilaya ya Arusha.
Taarifa hiyo
ya Ofisi ya Waziri Mkuu haikueleza sababu za kutenguliwa uteuzi wa Ntibenda
ambaye amekuwa Arusha tangu mwaka 2014.
Kwa mujibu
wa taarifa hiyo, Ntibenda, ambaye alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Karatu kabla ya
kuteuliwa kushika wadhifa huo mwaka 2014, amehamishiwa ofisi ya Waziri Mkuu
ambako atapangiwa kazi nyingine.
Jana,
Ntibenda alikuwa akisubiriwa kufungua mkutano wa shirika la kimataifa la afya
kwa vijana (AMREF) na tayari tangu asubuhi alikuwa ofisini kwake kujiandaa kwa
majukumu hayo ya siku.
Mbali na
mkutano huo, Ntibenda alitarajiwa kushiriki kama mwenyeji katika mkutano wa
Mfuko wa Maendeleo (Tasaf) ambao ulishirikisha wakuu wote wa mikoa ya Kanda ya
Kaskazini pamoja na wakuu wa wilaya.
Kwenye
mkutano wa AMREF, Ntibenda alisubiriwa kwa muda mrefu hadi habari za
kutenguliwa kwa uteuzi wake ziliposambaa, ndipo akateuliwa mganga mkuu wa mkoa,
Frida Mokiti kufungua mkutano huo.
Habari za
uhakika kutoka ofisi ya mkuu wa mkoa zinasema kuwa kabla ya kuibuka kwa taarifa
za kutenguliwa kwake, Ntibenda alikuwa na mazungumzo na Gambo ofisini kwake.
Haikujulikana
mara moja mambo waliyozungumza wawili hao, ingawa tangu Ntibenda ateuliwe kuwa
Mkuu wa Mkoa wa Arusha kumekuwa na utulivu wa kisiasa.
Ntibenda
alikuwa kwenye mzozo na viongozi wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), ambao
walikuwa wakimlalamikia kuingilia majukumu ya jumuiya hiyo.
Mwenyekiti
wa UVCCM wa mkoa, Lengai ole Sabaya aliwaambia waandishi wa habari mapema wiki
iliyopita wakati akisoma maazimo ya kamati ya utekelezaji, kuwa mkuu huyo
anakwamisha utendaji wao.
Katika
taarifa hiyo UVCCM ilisema kitendo cha Ntibenda kuingilia kati sakata la
mikataba ya wapangaji katika maduka ya jumuiya hiyo ni kuwakwamisha.
Baadaye
kundi la viongozi hao wa UVCCM pia lilidaiwa kuandika barua ya kumlalamikia
Ntibenda kutokana na kutoridhishwa na utendaji wake.
Hata hivyo,
Ntibenda alikanusha tuhuma zote za UVCCM kumtetea mmoja wa wapangaji na kusema
anasikitishwa na madai hayo dhidi yake.
Uteuzi wa
Gambo.
Wakati
Ntibenda akienguliwa, baadhi ya viongozi wa UVCCM jana walikuwa wenye furaha
baada ya Gambo kupandishwa cheo.
Mbunge wa
viti maalumu, Catherine Magige alimpongeza Rais Magufuli kwa uteuzi wa Gambo
ambaye alisema ni zao la jumuiya hiyo.
Magige
alisema uteuzi huo unaonyesha jinsi gani Rais Magufuli alivyo na imani na vijana
na akawataka kuendelea kumuunga mkono.
“Tunaamini
Gambo ataleta mabadiliko makubwa ya utendaji katika Mkoa wa Arusha kwa kuwa ni
mchapakazi,” alisema.
Wakati
Magige akisema hayo, Ole Sabaya alisema Rais Magufuli amesikia kilio chao.
“UVCCM
tulikuwa na malalamiko juu ya utendaji wa mkuu wa mkoa, sasa tunashukuru sana
Rais Magufuli kusikiliza kilio chetu,” alisema Ole Sabaya.
Kuondolewa
Ntibenda.
Lakini hali
ilikuwa tofauti kwa mbunge wa Arusha, Godbless Lema aliyesema anaona vurugu zikirudi
na kwamba uteuzi wa Gambo ni kama mkakati wa kuhakikisha wapinzani
wanasambaratishwa mkoani Arusha ambako ni moja ya ngome za Chadema.
Lema, ambaye
amekuwa katika mgogoro na Gambo katika siku za karibuni, alisema kada huyo
ameteuliwa ili kuidhibiti Chadema, jambo ambalo chama hicho hakitakubali.
“Hivi
karibuni nilimwambia mkuu wa mkoa Ntibenda kuna watu wanakutafuta, sasa
wamefanikiwa. Lakini mimi naona Arusha ijayo itakuwa na vurugu tofauti na
utulivu uliopo sasa,” alisema.
Hata hivyo,
alisema Chadema imejipanga kuendelea kufanya siasa za kistaarabu na kamwe
haitakubali kuhujumiwa na mtu yeyote yule.
Alipotafutwa
jana asubuhi, Gambo alisema hana cha kuzungumza na kwamba hakuwa na taarifa
rasmi.
Gambo,
ambaye jana alishiriki mkutano wa Tasaf kwa nafasi yake ya mkuu wa Wilaya ya
Arusha na baadaye kuondoka, alisema alikuwa hajapata taarifa rasmi.
Hata hivyo,
akiwa kwenye mkutano baadhi ya wakuu wa mkoa na wakuu wa wilaya za mikoa ya
Kanda ya Kaskazini, walimpongeza kwa uteuzi huo.
Katibu
Tawala wa Mkoa wa Arusha, Richard Kwitega alisema alipata taarifa za uteuzi huo
jana asubuhi na alipata maelekezo kuwa Gambo anatakiwa Dar es Salaam.
“Nilipata
taarifa rasmi ya uteuzi wake na tayari tulikuwa naye hapa ofisini ili kuweka taratibu
za kwenda kuapishwa,” alisema.
Alisema
Gambo atarejea Jumamosi na atapokewa na wafanyakazi na baadaye kushiriki
mapokezi ya Mwenge wa Uhuru wilayani Ngorongoro.
|
No comments:
Post a Comment