Rais John Magufuli anatarajia kufanya
ziara wilayani Kahama mkoani Shinyanga ambako atafanya mkutano wa hadhara
kuwashukuru wananchi kwa kumpigia kura nyingi katika Uchaguzi Mkuu uliopita.
Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Fadhili
Nkulu alisema jana,July 27, 2016 kwamba Rais Magufuli atawasili hapa Jumamosi
jioni kabla ya kufanya mkutano wa hadhara Jumapili.
Nkulu aliwataka wananchi wa Kahama na
maeneo jirani kujitokeza kwa wingi kumlaki kiongozi huyo katika ziara hiyo
ambayo alisema: “Lengo lake ni
kuwapongeza wananchi wa Kahama kwa kumpa kura nyingi katika Uchaguzi Mkuu
uliomalizika mwaka jana, 2015.”
Alisema ziara hiyo ni muhimu kwa kuwa
ni ya kwanza mkoani Shinyanga akianzia na Kahama.
“Tujipongeze
wananchi kutokana na kupata bahati ya wilaya chache zilizotembelewa na kiongozi
huyu, Kahama imekuwa mojawapo,” alisema Nkulu.
Alisema kwa kuwa Jumamosi ni siku ya
usafi kitaifa, kila mmoja wilayani humo ahakikishe anaweka mazingira katika hali
ya usafi na kuwaonya wafanyabiashara kuwa atakayeshindwa kufanya hivyo
hataruhusiwa kufungua biashara.
“Nitafanya
ukaguzi Jumamosi kuhakikisha kila mtu anashiriki usafi. Hilo ni agizo la
kitaifa kwa sasa lazima kila mmoja awajibike, nimewaagiza watendaji wote wa
kata kusimamia hilo,” alisema Nkulu.
Alisema wananchi watatangaziwa ratiba
yote ya Rais Magufuli kwenye gari la matangazo ambalo litazunguka mji mzima wa
Kahama kuwaeleza muda na eneo ambalo kiongozi huyo atafanyia mkutano.
|
No comments:
Post a Comment